Naibu Waziri wa Afya Dk. Kigwangalla azindua mkakati wa Taifa wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza Dodoma
FATILIA HOTUBA YA WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII ,JINSIA, WAZEE NA WATOTO MHE.DR HAMISI KIGWANGALLA.,
Hotuba ya Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dk. Hamisi Kigwangalla
Awali
ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetuwezesha kukusanyika
hapa siku ya leo. Pia, ninayo furaha kubwa kusimama mbele yenu kama
mgeni rasmi katika kuzindua mkakati huu muhimu wa pili wa kupambana na
magonjwa yasiyo ya kuambukiza. Pamoja na rasilimali chache tulizonazo,
Tanzania imepiga hatua kidogo katika kupambana na magonjwa yasiyo ya
kuambukiza.
Magonjwa
yasiyo ya kuambukiza yamekuwa yakiongezeka kwa kasi sana duniani na
haswa nchi zinazoendelea, Tanzania ikiwemo. Utafiti uliofanyika na
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa
kushirikiana na Shirika la Afya duniani na Taasisi ya NIMR, ya viashiria
vya magonjwa yasiyo ya kuambukiza imeonyesha kuongezeka kwa viashiria
hivyo.
Idadi ya watu wanaovuta sigara ni asilimia 15.9%, wanaokunywa pombe ni
asilimia 29.3%, wenye uzito uliopita kiasi 34.7%, shinikizo la damu ni
asilimia 25.9% na wagonjwa wa kisukari ni asilimia 9.1%. Hii
haikubaliki, na ni lazima tuongeze bidii katika kuyashughulikia.
Mkakati
huu umekuja wakati muafaka, wakati tunatakiwa kutekeleza Mpango wa
Malengo endelevu (Sustainable Development Goals) ambayo kati ya malengo
kumi na saba, matatu yanazungumzia jinsi ya kupambana na magonjwa yasiyo
ya kuambukiza, baadhi ya malengo haya ni;
- Kufikia mwaka 2030, kupunguza moja ya tatu ya vifo vitokanavyo na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa kukinga, kutibu na kuzingatia afya ya akili;
- Kuboresha huduma za kinga na tiba ya utumiaji wa madawa ya kulevya na pombe;
- Kufikia mwaka 2020, kupunguza nusu ya idadi ya vifo duniani na ajali za barabarani.
Napenda
kutambua mchango mkubwa uliotolewa na Chama cha kupambana na ugonjwa wa
kisukari duniani (World Diabetes Foundation) na chama cha kisukari cha
Tanzania (Tanzania Diabetes Association), kwa kuwezesha kupitiwa kwa
mkakati wa zamani wa mwaka 2008-2015, na kutengenezwa huu wa sasa, ambao
ni wa 2016-2020.
Kwa
kushirikiana na kitengo cha magonjwa yasiyo ya kuambukiza, TDA imeweza
kutekeleza mpango wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza nchi nzima.
Aidha
nawashukuru kwa dhati wadau wetu wa Maendeleo kwa misaada mbalimbali
ambayo imechangia katika kuboresha Afya za Watanzania.
Ninayo
taarifa kuwa Waganga wakuu wa mikoa na wilaya mmeombwa kuteua mtu mmoja
atakayeratibu shughuli zote za magonjwa yasiyo ya kuambukiza mikoani na
wilayani kwenu. Ni matarajio yangu kuwa mtafanya kazi kwa nguvu na kwa
ukaribu zaidi na kitengo cha magonjwa yasiyo ya kuambukiza cha Wizara
ili huduma hizi ziwafikie watu wote hadi ngazi ya jamii.
Baada
ya kusema haya machache , sasa natamka kuwa Mkakati huu wa pili wa
kitaifa wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza umezinduliwa rasmi.