SEKTA YA UVUVI IANGALIWE, TANZANIA
Na mwandishi wetu; Ada
Ouko,Musoma.
MCHANGO wa
sekta ya uvuvi katika pato la Taifa kwa mwaka 2015 ulikuwa ni asilimia 2.5
lakini takwimu zinaonesha kuwa katika mwaka huo sekta hiyo iliingizia serikali
mapato ya shilingi bilioni 12.9 kutokana na kusafirisha nje ya nchi kiasi cha
tani 40,540.95 za samaki na mazao ya uvuvi.
Pia kati ya
tani hizo ziwa victoria lilichangia zaidi ya tani 29,000 na kuingizia serikali
zaidi ya shilingi bilioni 11.3 ambayo ni asilimia 87.6 pato linalotokana na
sekta ya uvuvi katika kipindi cha mwaka 2015.
Hayo
yalielezwa juzi na katibu mkuu wizara ya kilimo,mifugo na uvuvi nchini Yohana
Budeba wakati alipokua akisoma hotuba yake na kufanya ufunguzi wa mkutano wa kuwasilisha
ripoti ya sensa ya uvuvi(frame Survey) ya mwaka 2016 mbele ya wadau wa sekta
hiyo kutoka mikoa ya kanda ya ziwa victoria.
‘’Ni ukweli
ulio wazi kwamba maendeleo ya wananchi katika Nyanja za kiuchumi na kijamii
yamekuwa yakitegemea sana shughuli za uvuvi katika halmashauri hizi, ni katika
muktadha huo,serikali kupitia idara za maendeleo ya uvuvi na ufugaji wa viumbe
katika maji imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa uvuvi katika ziwa victoria
unakuwa endelevu na wa manufaa zaidi’’alisema.
Budeba
alisema miongoni mwa madhumuni ya sensa hiyo ni kupata takwimu zinazohusiana na
nguvu ya uvuvi iliyopo katika mavuvi mbalimbali sambamba na hilo kupata idadi
ya mialo,idadi ya wavuvi,idadi ya aina ya vyombo vya uvuvi idadi na aina ya zana za uvuvi, na miundombinu
iliyopo katika mialo husika.
Kwa
kuzingatia hilo alisema ulinganisho wa takwimu za sensa za uvuvi zilizotangulia na sense ya sasa unaonesha
ongezeko kubwa la idadi ya wavuvi,vyombo na zana haramu wakati rasilimali
imekuwa ikipungua.
‘’Kwa mujibu
wa sensa iliyofanyika mwaka 2014 idadi ya wavuvi ilikuwa 103,540 lakini sensa ya
uvuvi iliyofanyika mwezi septemba 2016 idadi ya wavuvi waliopo imefikia 109,397
ambalo ni sawa na ongezeko la asilimia
5.7 vilevile idadi ya vyombo imeongezeka kutoka 29,154 vilivyopatikana katika sense
iliyofanyika mwaka 2014 na kufikia 31,773 katika sensa ya mwaka 2016 sawa na
ongezeko la asilimia 29’’alisema Budeba.
Kwa upande
wake kaimu mkurugenzi wa idara ya maendeleo ya uvuvi Magese Emmanueli aliwataka
maafisa uvuvi kutoka halmashauri za wilaya mbalimbali za mikoa ya kanda ya ziwa
kuzingatia sharia no.22 ya mwaka 2003 na kanuni zake za mwaka 2009 vizuri kwani
uvivi haramu ukitokea katika maeneo yao afisa husika atawajibika kwa mujibu wa sharia
hiyo.
Naye afisa
uvuvi katika manispaa ya Musoma Joseph Msuya alisema serikali iunde chombo
maalumu(fire patrol) na kutoa bajeti kwa ajili ya kuwakamata wavuvi haramu
sambamba na hilo asilimia 15 ya mapato yatokanayo na BMU irudishwe kuboresha
maslahi ya kamati ya ulinzi na usalama wa ziwa victoria.