Shinyanga yatajwa kuwa kinara kwa ndoa utotoni
Mkoa
wa Shinyanga umetajwa kuongoza nchini kwa kuwa na idadi kubwa ya ndoa
za utotoni kwa wasichana waliochini ya umri wa miaka 18.
Kaimu
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Watoto, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jinsia,
Wazee na Watoto, Magreth Mussai wakati akizungumza na waandishi wa
habari kuhusu Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Kike duniani yanayofanyika
Oktoba 11 kila mwaka, amesema takwimu zinaonyesha kuwa mkoa huo
unaongoza kwa asilimia 59.
Mussai
amesema kufuatia mkoa huo kukithiri ndoa za utotoni, ndiyo sababu ya
wizara ya afya kuuchagua kufanya maadhimisho hayo kitaifa.
Hata
hivyo, amesema mkoa unaofuata kwa kukithiri ndoa za utotoni ni Tabora
kwa asilimia 58, Mara 55, Dodoma 51 wakati Dar es Dalaam ikiwa na
asilimia 19.
Amesema
sababu inayopelekea familia nyingi kuwaoza mabinti zao chini ya umri wa
miaka 18 ni hali ngumu ya maisha na kwamba wazazi huitumia njia hiyo
kujipatia fedha kwa kupata mahali.
Mussai amesema serikali inaendelea kutoa elimu kwa jamii kutambua kuwa ndoa za utotoni zina athiri kiafya na kimwili watoto hao.
Ambapo ameitaka jamii kuwajibika ili kuhakikisha kwamba watoto wa kike hawaozeshwi chini ya umri wa miaka 18.