Jeshi la Polisi Dar laua majambazi saba katika matukio mawili tofauti
Kikosi
cha Kupambana na Ujambazi wa Kutumia Silaha cha Jeshi la Polisi Kanda
Maalumu ya Dar es Salaam juzi katika tukio la majibizano ya risasi baina
ya majambazi na polisi maeneo ya Mbezi kwa Yusuph Makondeni kiliwauwa
watu 6 waliotuhumiwa kuwa majambazi.
Kaimu
Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam DCP, Lucas Mkondya
wakati akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam,
amesema kabla ya tukio hilo kutokea, polisi walipata taarifa kutoka kwa
raia wema kuwa kuna kikundi cha watu wenye silaha kimejipanga kufanya
tukio la ujambazi wa kutumia silaha kwa mfanyabiashara aliyekuwa akitoka
benki ya DTB tawi la Nyerere road na kwamba angepita katika barabara
hiyo waliyokuwepo majambazi hao.
Amesema
baada ya polisi kupata taarifa hiyo, waliwawekea mtego majambazi hao,
na kubaini kuwa walikuwa wanalifukuza gari la mfanyabiashara huyo.
Ameeleza
kuwa, baada ya majambazi kugundua wameingia katika mtego wa polisi
walianza kufyatua risasi ndipo polisi nao wakajibu mashambulizi.
Amesema miili ya majambazi hao iko katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Katika
tukio lingine, DCP Mkondya amesema Terehe 17, 9, 2016 maeneo ya Tegeta
Masaiti majambazi watatu wakiwa na silaha walivamia duka la Abdallah
Juma na kupora fedha za mauzo. Na kwamba polisi baada ya kupata taarifa
waliwafukuza majambazi hao hata hivyo wananchi wenye hasira kali
waliwakimbiza na kumuua jambazi mmoja huku waliobaki walifanikiwa
kukimbia.