UKARABATI WA KABURI LA MWALIMU NYERERE WAKAMILIKA



Msaidizi wa Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Fedson Masawa (kushoto) akitoa maelekezo wakati wa zoezi la kunyunyizia dawa ya kuua wadudu kwenye paa la nyumba lilipo kaburi la Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere. Kulia ni William Elisha ambaye ni mmoja wa wanafamilia akiwa na mtaalamu aliyefanya zoezi hilo.

Na Mwandishi Wetu

UKARABATI wa kaburi la Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere umekamilika, ambapo shughuli zilizofanyika ni upakaji wa rangi, unyunyiziaji dawa kwenye paa la nyumba ya kaburi hilo pamoja na kupaka rangi kwenye mawe yaliyomo kwenye nyumba aliyokuwa akiishi Mwalimu Nyerere.

Akizungumza kwa niaba ya familia ya Mwalimu Nyerere mara baada ya kukamilika kwa ukarabati huo, mzee Iddi Selemani alishukuru ushirikiano uliotolewa na Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini katika kuhakikisha zoezi hilo linakamilika.

Mzee Selemani alisema, anaamini mahusiano ya familia ya Mwalimu Nyerere na viongozi mbalimbali wa nje na ndani ya Tanzania yataendelea kudumu daima na wao kama wanafamilia wataendelea kutoa ushirikiano mkubwa kwa kiongozi yeyote atakayefika kijijini hapo.

“Kwa niaba ya familia ya Mwalimu Nyerere, nitoe shukrani zangu nyingi kwa Prof. Muhongo kupitia ofisi yake kwa namna tulivyoshirikiana katika kulifanikisha zoezi hili. Nasi kama familia tutaendelea kutoa ushirikiano mkubwa kwa kiongozi yeyote atakayetutembelea ili kuendeleza mahusiano aliyokuwa nayo Mwalimu iwe ndani hata nje ya Tanzania” alisema mzee Idd Selemani.

Kwa upande wake Fedson Masawa akizungumza kwa niaba ya Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Prof. Sospeter Muhongo alishukuru kwa ushirikiano aliopata kutoka kwa familia hiyo ambao umechangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha zoezi hilo litakalosaidia kuendeleza mahusiano baina ya viongozi mbalimbali wa serikali na familia zao.
Powered by Blogger.