KIWANDA KIKUBWA CHA CHAKI KUJENGWA MASWA.


 
Na mwandishi wa MAKALIBLOG.
 COSTANTINE MATHIAS; SIMIYU.
KUFUATIA Agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. John Pombe Magufuli la kuwa na Tanzania ya Viwanda, Mkoa wa Simiyu unatarajia kujenga kiwanda kikubwa cha chaki kikiwa na teknolojia mpya katika Ukanda wa Afrika Mashariki ambacho kitasaidia kuongeza ajira na kukuza uchumi wa mkoa na taifa kwa ujumla.

 kiwanda hicho ambacho kitakuwa na teknolojia ya kisasa zaidi katika uchanganyaji unga, uzalishaji na ufungashaji kitaongeza ajira kwa vijana wilayani Maswa ambao alikuwa wameanza na kiwanda kidogo kilichokuwa kikizalisha kwa kutumia teknolojia duni.

Hayo yalibainishwa jana na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka katika Kikao cha Baraza la Madiwani mjini Maswa wakati akifafanua mikakati ya mkoa katika kutekeleza azma ya serikali ya viwanda.
 
Mtaka alisema kuwa kwa kuwa kiwanda kikubwa kinatarajiwa kujengwa Maswa Halmashauri ianze kufikiria kumiliki vitalu vyake vya chokaa ambapo hadi sasa wanamiliki ekari 20 ambazo zitasaidia kulisha kiwanda hicho wakati wa uzalishaji ili kisikose malighafi.

‘’tunajenga kiwanda kipya kikubwa cha chaki na cha kisasa ambacho hakipo Afrika Mashariki…na shilingi milioni 50 zimeshatolewa na UNDP kwa ajili ya upembuzi yakinifu’’ alisema Mtaka.

Aliongeza kuwa kiwanda hicho kitakuwa na teknolojia ya kisasa katika uzalishaji wake huku ujenzi wake utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 1.5 zilizotolewa na mfuko wa Hifadhi ya jamii (NSSF).

Aidha Mtaka ameziagiza halmashauri zote mkoani hapa kubuni vyanzo vipya vya mapato  hasa kwa kuanzisha viwanda vidogovidogo na vikubwa ili waachana na tabia ya kuwatoza  ushuru wakulima wakulima wa mazao mashambani.

‘’halmashauri zibuni vyanzo vipya vya mapato na siyo kufikiria kutoza ushuru wauza michicha na nyanya sokoni…mfano halmshauri ya Maswa leo imepokea milioni 70 toka Zanzibar baada ya kuuza chaki na bado wanadai milioni 200’’ alisisitiza Mtaka.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya  Wilaya ya Maswa Dr. Fredrick Sagamiko alisema kuwa hadi sasa wilaya yake imeanza mchakato wa ujenzi wa kiwanda cha kuongeza thamani ya mazao ya ngozi.

Alisema kuwa kiwanda hicho  kinajengwa katika kijiji cha Senani chini ya ubia wa wajasiriamali Kijijini hapo, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo-SUA na Chuo cha Teknolojia -DIT  ambapo ujenzi wake utakamilika mwezi Julai mwaka huu.

‘’ujenzi wa kiwanda cha kuongeza thamani ya mazao ya ngozi unandelea, pia tumeanza kusajili na kutambua mifugo yote wilayani maswa ambapo wananchi wameitikia zoezi la upigaji chapa mifugo yao’’ alisema Sagamiko.

Aidha Kwa upande wao wananchi wamesema kuwa agizo la Mkuu wa mkoa la kufutwa kwa ushuru wa mazao litasaidia halmashauri kubuni miradi na vyanzo vingine vya mapato kuliko kutegemea ushuru wa sokoni.

‘’ni kweli watasaidia hata wataalamu kubuni miradi ambayo itakuwa vyanzo vya mapatoa katika halmashauri kuliko kutegemea ushuru wa minadani, sokoni, mazao na stendi’’ alisema Juma Ally.
 
 
MWISHO
Powered by Blogger.