MAMA MJAMZITO ALIYEANGUKIWA NYUMBA ATEMBELEWA NA MSAIDIZI WA MBUNGE MUSOMA VIJIJINI



Msaidizi wa Mbunge Fedson Masawa (kulia) akiwa amembeba mtoto wa Roza Nyangasi (aliyekaa), kushoto ni Tabu Munibhi ambaye ni wifi wa Roza na mmoja wa watu wanaomuuguza mgonjwa huyo.

Na. Mwandishi Wetu MARA
MMOJA wa majeruhi aliyeangukiwa na nyumba kufuatia mvua kubwa na upepo mkali uliovikumba vijiji mbalimbali vya Jimbo la Musoma Vijijini Roza Nyangasi mkazi wa kitongoji cha Stoo kijiji cha Kurukerege kata ya Nyegina amesema anaendelea vizuri baada ya kupata matibabu.

Roza ambaye wakati anapatwa na ajali hiyo alikuwa mjamzito amefanikiwa kujifungua mtoto wa kike anayeitwa Rehema na anaendelea vizuri.

Akizungumza na msaidizi wa mbunge Fedson Masawa aliyemtembelea kujua maendeleo yake, Roza alimshukuru Prof. Sospeter Muhongo kwa mchango wake ambao umemsaidia kugharamia matibabu na hadi sasa anaendelea vizuri.

“Namshukuru Mungu naendelea vizuri japo bado kuna maumivu sehemu za shingo ambapo matofali yalinidondokea. Lakini pia shukrani nyingi sana zimuendee Mbunge wangu Prof. Muhongo kwani bila mchango wake hali yangu ya matibabu haya ingekuwa mbaya” alisema na kushukuru Roza ambaye baada ya kuangukiwa na matofali aliumia miguuni huku akiwa mjamzito na baada ya siku nne alijifungua.

Awali, Kabla ya kuwasili katika kijiji cha Kurukerege kata ya Nyegina, msaidizi huyo wa mbunge aliendelea na zoezi maalum la kufanya tathimini ya uharibifu wa nyumba uliosababishwa na kimbunga na kubahatika kufika nyumbani kwa Roza Nyangasi.

Mapema mwezi uliopita, Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo alimtembelea mama huyo na kumsaidia mchango wa shilingi 200,000 kwa ajili ya huduma ya matibabu ambazo anakiri zimemsaidia kwa kiasi kikubwa.
Powered by Blogger.