KANISA LA advetist KAMUNYONGE MUSOMA WASHIRIKI KUWAOMBEA WANAFUNZI WA LUCK VICENT WALIOPARTA AJALI

 
Serikali mkoani Mara imeyahakikishia madhehebu mbalimbali ya kidini kwamba itaendelea kushirikiana nayo kutokana na mchango wake mkubwa katika kudumisha amani na umoja wa Watanzania ulioasisiwa katika taifa hili na Baba wa Taifa Marehemu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
 
Kauli hiyo imetolewa hapo Mei 20 mwaka huu na Mkuu wa mkoa wa Mara Dk Charles Mlingwa wakati alipowaongoza maelfu ya waumini wa Kanisa Kuu la Waadventista Wasabato (SDA) la Kamunyonge lililopo mjini Musoma katika ibada maalum ya kuwaombea majeruhi wa ajali ya wanafunzi iliyotokea wilayani Karatu mkoani Arusha Mei 6 mwaka huu.
 
Dk Mlingwa katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala wa wilaya ya Musoma Justine Manko amesema madhehebu ya dini yameendelea kutoa mchango mkubwa wa kudumisha amani,upendo,umoja na mshikamano miongoni mwa Watanzania huku pia yakileta maendeleo kwa wananchi kupitia huduma mbalimbali katika sekta za Afya,Elimu,Maji na Uchumi.
 
Amesema ni kwa msingi huo serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dk John Magufuli imeendelea kushirikiana na madhehebu hayo ya kidini katika kuhakikisha kwamba wananchi wanafanya kazi zao za kimaendeleo kutokana na amani iliyodumu hapa nchini baada ya kuasisiwa kwake na marehemu Mwalimu Nyerere tangu nchi ilipopata uhuru wake hapo Desemba 9 mwaka 1961.
 
Kwa upande wake Mchungaji wa kanisa hilo la Waadventista Wasabato toka mkoani Dodoma David Mbaga aliyeendesha ibada hiyo maalum, alimuomba Mwenyezi Mungu kuleta uponyaji kwa majeruhi kupitia kwa madaktari wa Hospitali ya Mercy iliyopo Jiji la Sioux, IOWA nchini Marekani ambapo wanaofanya matibabu ya kina ya mifupa kutokana na majeraha waliyopata ikiwamo kuvunjika mifupa ya miguu, mkono, taya, shingo na nyonga.  
 
Mchungaji Mbaga ambaye pia aliendesha semina ya wiki moja ya watu kumjua Mungu sambamba na elimu ya ujasiriamali katika kanisa hilo Kuu la SDA la Kamunyonge tangu Mei 14 hadi Mei 20 mwaka huu, alisema ajali hiyo ya wanafunzi wa shule ya Msingi Lucky Vincent iliyoua watu 35, imeleta majonzi makubwa kwa familia,ndugu na jamaa za marehemu waliopoteza maisha katika ajali hiyo.
 
Ibada hiyo pia ilihudhuriwa na wageni mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Musoma Daudi Misango, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Musoma (MUWASA) Said Gantala, viongozi na waumini wa madhehebu mbalimbali ya kidini wakiwemo wachungaji.
 
Powered by Blogger.