DKT TIZEBA AMALIZA ZIARA YA KIKAZI MKOANI SINGIDA ATUA TABORA


Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akizungumza kwenye kikao kazi katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida. Picha Zote Na Mathias Canal, WK.
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu (Kushoto) na Mkuu wa Wilya ya Singida Mhe Elias Tarimo wakifatilia kikao cha kazi kilichoongozwa na waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba,
Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe Dkt. Rehema Nchimbi akizungumza jambo mbele ya waziri wa kilimo Mhe Dkt. Charles Tizeba alipotembelea ofisi ya Mkoa akiwa katika ziara ya kikazi ya siku mbili, 
Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akizungumza kwenye kikao kazi katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida. 

Na Mathias Canal-WK, Tabora

Waziri wa kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba amemaliza ziara ya kikazi ya siku mbili Mkoani Singida na tayari amewasili mkoani Tabora kwa ziara ya kikazi ya siku moja hapo kesho 10 Juni 2018.

Akiwa Mkoani Singida Mhe Dkt. Tizeba ametembelea vituo mbalimbali vya ukusanyaji wa pamba na kujionea msimu wa ununuzi wa pamba katika Wilaya ya Ikungi na Iramba.

Miongoni mwa mambo ya msisitizo katika maeneo yote hayo ni pamoja na kuwashauri wakulima kutouza pamba chafu kwa kudhani kuwa watapata kilo nyingi kwani jambo hilo linafifihisha soko la zao hilo kwa wanunuzi.

Katika hatua nyingine ametoa onyo kwa viongozi wa vyama vya ushirika AMKOS kutojihusisha na ubadhilifu wa fedha za wakulima huku akielekeza kukamatwa na kufikishwa mahakamani kwa wale wote waliobainika kuiba fedha za wakulima katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, ametangaza neema kwa wakulima wa pamba kote nchini kuwa msimu ujao wa kilimo wa mwaka 2018/2019 wakulima watapatiwa mbegu na dawa bure pasina malipo.

Akiwa katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Tizeba amewasisitiza watendaji wote mkoani humo kutoa ushirikiano mahususi kwa wakulima ili kuongeza tija katika uzalishaji wa zao la pamba na mazao mengine yakiwemo mahindi, mtama, alizeti N.k

Zao la pamba ni miongoni mwa mazao ya biashara yanayolimwa katika mkoa wa Singida, Katika msimu huu wa mwaka 2017/2018, mkoa ulipokea mbegu bora za pamba aina ya UKM 08 tani 381.48 na kusambazwa kwa wakulima ambapo jumla ya ekari 35,889 zilipandwa. Aidha, sumu chupa 137,970 zimesambazwa kwa wakulima na mabomba ya kunyunyizia sumu 365 yamesambazwa pia.

Pia amesisitiza kuwa uongozi wa mkoa huo unapaswa kujipanga kikamilifu kusimamia ununuzi wa pamba kupitia utaratibu uliowekwa wa kuvitumia Vyama vya Ushirika vya Kilimo na Masoko (AMCOS) pamoja Vyama vya Awali vya Ushirika  (Pre Cooperative Societies).

Katika mkoa huo jumla ya AMCOS 36 na “Pre Cooperatives” 20 zitahusika katika ununuzi wa zao la pamba katika msimu huu wa kilimo wa mwaka 2017/2018.

Akizungumza katika mkutano huo Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Dkt Rehema Nchimbi alisema kuwa mkoa huo ulikuwa na matarajio ya awali ya mavuno kwa tani 21,533.4 ambapo matarajio haya yameshuka mpaka kufikia tani 14,015.2 zinazotarajiwa kuvunwa kutokana na athari za wadudu waharibifu.

Alisema jumla ya vituo vitakavyotumika kukusanya na kununua pamba ni 117 ambavyo vimesambaa katika maeneo yote yanayolima pamba yaliyopo katika Halmashauri saba za Mkoa huo.

Aliongeza kuwa maghala yatakayotumika kununulia pamba katika vituo hivyo  yamesafishwa na kufukiziwa sumu ya kuuwa wadudu. Kampuni iliyoruhusiwa kununua pamba katika Mkoa huo ni BioSustain (T) LTD ambayo ni mdau mkubwa wa kilimo cha zao la pamba katika mkoa wa Singida kwani imewekeza kiwanda cha kuchambua pamba kilichopo Manispaa ya Singida.

MWISHO.
Powered by Blogger.