Waingereza watoa msaada kwa wakimbizi 236,000

Ni
 kutokana na mchango mkubwa wa Paundi za Uingereza milioni 1 (Dola za 
Marekani milioni 1.3) kutoka katika Shirika la Misaada la Uingereza 
(Department for International Development –DFID), kwamba Shirika la 
Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) limeweza, walau kwa 
muda, kusitisha mpango wa kupunguza kiasi cha mgao wa chakula uliopangwa
 kwa ajili ya wakimbizi nchini Tanzania.
WFP
 ilikuwa imepanga kupunguza kiasi cha mgao kuanzia Oktoba kwa karibu 
robo milioni ya wakimbizi kutokana na kukosekana kwa fedha za kuendeshea
 shughuli za WFP za kuhudumia wakimbizi nchini Tanzania. Sasa – walau 
kwa muda huu – shughuli hizi zitaendelea kama kawaida.
“Uingereza
 inaungana na Umoja wa Mataifa na jumuiya ya kimataifa katika kusaidia 
ukarimu mkubwa wa Serikali na watu wa Tanzania wa kuwakaribisha wale 
wanaotafuta usalama kutokana na mapigano nchini Burundi na ukanda wa 
Maziwa Makuu,” alisema Vel Gnanendran, ambaye ni Mkuu wa DFID. “Kwa 
hiyo, tunatoa mchango wa nyongeza mara moja wenye thamani ya Paundi 
milioni 1 ili kuisaidia WFP kuendelea kutoa chakula kwa idadi inayokuwa 
ya wakimbizi wanaowasili nchini Tanzania. Nyongeza hii inafanya jumla ya
 mchango wetu kwa WFP kufikia Paundi milioni 6.5 tangu mgogoro huu 
uanze.”
Wakimbizi wakigaiwa msaada wa chakula kwenye kambi zao. (Picha zote na Tala Loubieh wa WFP).
WFP
 husambaza chakula kinachookoa maisha kwa wakimbizi wapatao 236,000 
wanaoishi katika kambi tatu mkoani Kigoma, kaskazini magharibi mwa 
Tanzania. Wakimbizi wanategemea msaada huu, ambao ni pamoja na mahindi, 
kunde, mafuta ya kupikia, chumvi na mchanganyiko wa uji wenye 
virutubisho.
“WFP
 inatoa shukrani za dhati kwa DFID kwa mchango wao katika kipindi hiki 
muhimu,” alisema Michael Dunford, Mwakilishi wa Nchi wa WFP nchini 
Tanzania. “Wakati ambapo fedha zaidi za nyongeza zinahitajika haraka ili
 kukidhi mahitaji ya wakimbizi hadi kufikia mwisho wa mwaka huu, 
tunathamini sana mchango huu mkubwa.”
Licha
 ya kuhakikisha upatikanaji wa mahitaji ya kikalori ya kila siku ya 
wakimbizi, WFP hutoa chakula kilichopikwa katika vituo vya mpito na 
kupokelea wakimbizi na vituo vya afya. Katika kambi za wakimbizi, WFP 
pia husaidia akina mama wajawazito na wale wanaonyonyesha, na pia watoto
 wenye utapiamlo wa kiwango cha kati walio na umri wa chini ya miaka 
mitano kwa kuwapatia unga wenye virutubisho au mchanganyiko wa uji 
ulioongezewa virutubisho.
Wakimbizi wakigaiwa msaada wa chakula kwenye kambi zao. (Picha zote na Tala Loubieh wa WFP).
Kila
 siku, mamia ya wakimbizi kutoka Burundi huwasili katika mpaka wa 
Tanzania, hasa kutokana na kuendelea kwa mapigano nchini mwao. WFP 
inamudu kutimiza wajibu wake kutokana na misaada itokayo kwa wahisani. 
Lakini kutokana na kuendelea kumiminika kwa wakimbizi, Shirika lina hali
 ngumu ya kifedha. Michango isipoongezeka, usalama wa chakula na lishe 
wa wakimbizi unaweza kuwa katika hatari kubwa.
Ili
 kuendeleza shughuli za kuwahudumia wakimbizi hadi mwisho wa mwaka, WFP 
inahitaji Dola za Marekani milioni 7.6. Jumla ya Dola za Marekani 
milioni 63.6 zinahitajika hadi kufika Agosti, 2017.