MWENYEKITI WA WAENDESHA BODABODA MANSPAA YA SHINYANGA AJIUA KWA KUJINYONGA

Mwenyekiti wa waendesha bodaboda 
shinyanga Jacob Paul amejiua kwa kujinyonga mchana huu katika eneo la 
Mapinduzi Ngokolo mjini Shinyanga.
Askari polisi
 wakiweka kwenye gari la polisi mwili wa Mwenyekiti wa chama cha 
waendesha pikipiki manispaa ya Shinyanga Jacob Paul aliyejiua leo Juni 
10,2017 kwa kujinyonga nyumbani kwake huku chanzo kikihusishwa na 
mgogoro wa waendesha bodaboda na jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga****
 
Mamia ya wakazi wa Shinyanga wamepigwa 
butwaa baada ya mwenyekiti wa chama cha waendesha pikipiki maarufu 
bodaboda katika manispaa ya Shinyanga Jacob Paul (36) kujiua kwa 
kujinyonga kwa kutumia waya wa simu chumbani kwake. Mwandishi mkuu wa 
Malunde1 blog,Kadama Malunde anaripoti.
Tukio hilo la kushangaza limetokea 
Jumamosi Juni 10,2017 majira ya saa nane mchana katika mtaa wa Mwinamila
 kata ya Ngokolo katika manispaa ya Shinyanga.
Mashuhuda wa tukio hilo walisema Jacob 
Paul ambaye ni mwenyeji wa mkoa wa Kigoma alifika nyumbani kwake leo 
majira ya saa saba mchana akiwa amepakizwa kwenye pikipiki na mwendesha 
bodaboda mwenzake huku akionekana kuwa mtu mwenye furaha kisha akaingia 
ndani kwake.
Walieleza kuwa baada ya takribani dakika
 30 watoto wawili marehemu walifika nyumbani wakitaka kuingia ndani ya 
nyumba lakini mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani walijaribu kumuita 
lakini hakujibu ndipo wakaamua kwenda kuchungulia dirishani.
Walifafanua kuwa watoto hao 
walipochungulia dirishani walimuona baba yao akiwa amening’inia chumbani
 kisha kutoa taarifa kwa majirani na baba mwenye nyumba akaamua kutoa 
taarifa kwa jeshi la polisi.
“Mke wa 
marehemu hakuwepo tulipoona kuwa mlango ni mgumu kufunguka tuliamua 
kuuvunja na kumkuta amejiua na huenda chanzo cha kifo chake kimetokana 
na msongo wa mawazo kwa sababu tangu kutokea kwa tukio la mwendesha 
bodaboda Joel Gabriel Mamla (26) kufariki dunia,alikuwa anasema 
waendesha bodaboda wenzake wamekuwa wakimlalamikia kuwa anashirikiana na
 polisi kukamata waendesha bodaboda waliofanya vurugu hivi karibuni”,alieleza jirani Sarah Edward.
“Jana 
alikuwa anasema kuwa anapewa vitisho na wenzie kuwa anawasaliti na 
kusababisha waendesha wakamatwe na polisi na pikipiki zao”,alieleza jirani huyo.
“Nilikwambia
 mme wangu ujiuzulu uenyekiti,ona sasa waendesha bodaboda wenzako 
wamekuponza,wamekusababishe ujiue baba Joshua,umeacha familia yako 
bora,watoto hawa watalelewa na nani”, mke wa marehemu Rebeca Amos aliyekuwa analia muda wote wakati wa tukio alisikika akiongea kwa uchungu.
Alisema mme wake amekuwa akipokea vitisho kwa watu wasiojulikana wakimtuhumu kuwasaliti na kusababisha wakamatwe.
Habari kutoka eneo la tukio zinasema 
kuwa marehemu alikuwa analalamikiwa na waendesha bodaboda wenzake kuwa 
anashirikiana na jeshi la polisi kugandamiza waendesha bodaboda wenzake.
“Mwenyekiti anadaiwa kuwasaliti 
wenzake,hata kipindi kile mwendesha bodaboda Boaz William aliyefariki 
dunia kwa kugongwa gari wakati akidaiwa kuwakimbia askari wa usalama 
barabarani mjini Shinyanga anadaiwa kushirikiana na polisi kutorosha 
mwili wa marehemu na kuupeleka Kigoma kwa ajili ya mazishi ambapo hata 
waendesha bodaboda hawakupata hata nafasi ya kuaga mwili wa 
marehemu”,ilielezwa Malunde1 blog.
Diwani wa kata ya Ngokolo,Emmanuel Ntobi
 alifika eneo la tukio alimuomba rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
 Dkt. John Pombe Magufuli kuunda tume huru ya kijaji kuchunguza vifo vya
 waendesha bodaboda katika manispaa ya Shinyanga.
“Sasa 
idadi ya vifo vya waendesha bodaboda vimetokea Shinyanga,kuna utata 
kwani jamii inasema vifo vinasababishwa na askari polisi huku jeshi la 
polisi nalo likidai waendesha bodaboda ndiyo wanasababisha vifo vyao kwa
 kukiuka sheria za usalama barabarani,mpaka sasa pikipiki nyingi 
zimekamatwa”,alieleza Ntobi.
Kamanda wa jeshi la polisi ACP Muliro 
Jumanne Muliro aliyekuwepo eneo la tukio alisema wamekuta mwenyekiti 
huyo wa waendesha bodaboda amejinyonga kwa kutumia waya mgumu wa simu 
katika chumba chake.
“Tumepata taarifa kuhusu tukio 
hili,tulipofika tumekuta amefariki kwa kujing’iniza kwa waya,tumeuchua 
mwili wa marehemu kwa ajili ya kuufanyia uchunguzi hospitalini,sisi kazi
 yetu ni kuchunguza chanzo cha kifo,bado tunafanya uchunguzi zaidi juu 
ya tukio hili tutatoa taarifa zaidi baadaye”,alisema kamanda Muliro.
Tukio la mwenyekiti wa waendesha 
bodaboda kujiua limetokea siku tano tu baada ya jeshi la polisi mkoani 
Shinyanga,kulazimika kuwapiga mabomu ya machozi waendesha bodaboda, kwa 
kitendo cha kuundamana kupinga kifo cha mwenzao Joel Gabriel Mamla 
(26),kilichodaiwa kusababishwa na askari polisi PC Edmund baada ya 
kumkamata kwa kosa la kutovaa helmet. SOMA <<HAPA>>
Kwa mujibu wa jeshi la polisi watu 26 
walifikishwa katika mahakama ya wilaya ya Shinyanga kwa mashtaka ya 
kufanya mkusanyiko usio halali,kufanya fujo na kujaribu kufanya 
maandamano kinyume na sheria.
Kati yao David Laurent alikiri kosa lake
 na kuhukumiwa kifungo cha miezi sita jela na wengine kesi yao 
iliahirishwa na itaendelea Julai 23,2017.
HII HAPA TAARIFA YA JESHI LA POLISI KUHUSU WAENDESHA BODABODA KUFIKISHWA MAHAKAMANI.
TAARIFA YA JESHI LA POLISI MKOA WA SHINYANGA KWA VYOMBO VYA HABARI TAREHE 10/06/2017 
TAREHE 09/06/2017 WATU 26 WALIFIKISHhWA 
KATIKA MAHAKAMA YA WILAYA YA SHINYANGA NA KUFUNGULIWA KESI YA JINAI NO 
134 NA BAADAE KUSOMEWA MASHITAKA YA KUFANYA MKUSANYIKO USIOHALALI , 
KUFANYA FUJO NA KUJARIBU KUFANYA MAANDAMANO KINYUME NA SHERIA.
MAKOSA HAYO WALIYATENDA TAREHE 
07/06/2017 MAJIRA YA SAA 04.30 ASUBUHI WAKATI KUNDI LA WATU WAPATAO 80 
WENGI WAO WAKIWA NI WAENDESHA PIKIPIKI MAARUFU KAMA BODABODA WAKIWA ENEO
 LA IBINZAMATA MANISPAA YA SHINYANGA KWA PAMOJA WALIKUSANYIKA WAKAPANGA 
NA KUFANYA MAANDAMANO KINYUME NA SHERIA NA KUANZA KUYARUSHIA MAWE BAADHI
 YA MAGARI NA KUSABABISHA USUMBUFU KWA BAADHI YA RAIA NA WATUMIAJI 
WENGINE WA BARABARA NA HIVYO KUJENGA HOFU NA KUPELEKEA KUVUNJIKA KWA 
AMANI KATIKA ENEO HILO. 
MTUHUMIWA MMOJA NO 18 KATIKA HATI HIYO 
YA MASHITAKA AITWAYE DAVID LAURENT ALIKIRI KOSA LAKE BAADA YA KUSOMEWA 
MASHTAKA HAYO NA MWANASHERIA WA SERIKALI CAROLINE MUSHI MBELE YA HAKIMU 
DENIS LUWUNGO. 
MTUHUMIWA HUYO AMEHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIEZI SITA JELA NA WENGINE KESI YAO IMEAHIRISHWA NA ITAENDELEA TAREHE 23/06/2017. 
WAKATI HUOHUO IMETOKEA AJALI YA PIKIPIKI
 NA KUSABABISHA KIFO. TAREHE 10/06/2017 SAA 08 USIKU BARABARA YA MAGANZO
 ENEO LA MATANDA SISI KWA SISI ZONE 1 MWENDESHA PIKIPIKI SHINJE MACHIYA 
MKAZI WA BUGWETO AKIWA NA PIKIPIKI NO MC 303 HUKU AKIIENDESHA KWA KASI 
NA BILA KUWA NA KOFIA NGUMU HELMET ALIPATA AJALI BAADA YA KUANGUKA NA 
KUFARIKI PALEPALE BAADA YA KUVUJA DAMU NYINGI KICHWANI.
CHANZO CHA KIFO HICHO NI MWENDO KASI , 
KUTOVAA HELMET NA KUPELEKEA AJALI ILIYOSABABISHA KUVUJA KWA DAMU NYINGI 
KICHWANI NA HATIMAYE KUFA. MWILI WA MAREHEMU UMEHIFADHIWA HOSPITALI YA 
RUFAA YA MKOA WA SHINYANGA.
IMETOLEWA NA MULIRO J MULIRO (ACP) - RPC SHINYANGA.
Angalia picha hapa chini
Kamanda wa jeshi la polisi ACP Muliro Jumanne Muliro (wa tatu kutoka kushoto) akiwa nyumbani kwa marehemu Jacob Paul
Wananchi wakiwa nyumbani kwa marehemu Jacob Paul
Kamanda wa jeshi la polisi ACP Muliro Jumanne Muliro akisikiliza maelezo kutoka kwa mke wa marehemu,bi Rebeca Amos
Kamanda wa Jeshi la polisi mkoa wa 
Shinyanga ACP Muliro Jumanne Muliro akielekea kwenye chumba cha marehemu
 Jacob Paul akiwa ameambatana na maafisa wa jeshi la polisi huku ulinzi 
ukiwa umeimarishwa 
Askari polisi wakiimarisha ulinzi nyumbani kwa marehemu Jacob Paul
Mke wa marehemu akilia kwa uchungu wa kupoteza mme
Wananchi wakiwa eneo la tukio
Wananchi wakiwa nyumbani kwa marehemu Jacob Paul
Askari polisi wakiwa wamebeba mwili wa marehemu Jacob Paul
Askari polisi wakiwa wamebeba mwili wa marehemu
Mwili wa marehemu ukiwekwa kwenye gari la polisi
Askari polisi wakiondoka na mwili wa marehemu
Jirani yake na marehemu,Sarah Edward akielezea tukio hilo
Diwani wa kata ya Ngokolo Emmanuel Ntobi
 akizungumza na waandishi wa habari kuhusu tukio la mwenyekiti wa 
waendesha bodaboda manispaa ya Shinyanga,Jacob Paul aliyejiua kwa 
kujinyonga
picha kwa hisa ya malunde. 

 
 
 
 
 
